Advertisements

Wednesday, August 24, 2016

MBOWE KUNYANG’ANYWA BILICANAS MWEZI HUU

Zimebaki wiki tatu kabla Shirika la Nyumba la Taifa (NHC) kuchukua jengo la Bilicanas lililokodiwa na Mwenyekiti wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), Freeman Mbowe, kuendesha biashara ya ukumbi wa starehe.


Jengo hilo lipo eneo la Posta jijini Dar es Salaam.Awali, NHC ilikuwa imetoa notisi ya siku 60 kwa wadaiwa sugu ambao wamepanga katika majengo yake akiwamo Mbowe.

Akizungumza na waandishi wa habari jana, Mkurugenzi Mkuu wa NHC, Nehemia Mchechu, alisema pamoja na Bilicanas, shirika linazidai taasisi za umma, binafsi na watu binafsi jumla ya Sh. bilioni 15.

Notisi ya siku 60 ya kuondoka Bilicanas pamoja na majengo ya wadaiwa wengine ilishatolewa, Mchechu alisema na kwamba sasa zimesalia wiki tatu.

Alisema baada ya muda huo kumalizika, utekelezaji wa kuondolewa katika majengo hayo utaanza ukiambatana na uchukuaji wa hatua za kisheria.

Mchechu alisema mbali ya Bilicanas, wadaiwa wengine ni Wizara ya Mawasiliano na Uchukuzi inayodaiwa Sh. bilioni mbili, Benki ya Azania (Sh. milioni 161) na Wizara ya Mambo ya Nje, Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Kikanda na Kimataifa (Sh. milioni 631).


Wadaiwa wengine walitajwa kuwa ni Wizara ya Afya na Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto (Sh. bilioni 1.3), Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano (Sh. bilioni mbili), Tume ya Utumishi (Sh. milioni 109) na Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo Sh. bilioni moja.

Mchechu alisema ukusanyaji wa madeni hayo kwa nguvu ni mkakati wa shirika hilo kukusanya fedha ili kusaidia ujenzi wa nyumba za watumishi wanaohamia Dodoma.

Alipoulizwa iwapo mkakati huo una uhusiano wowote na masuala ya kisiasa kutokana na kumtaja Mbowe kuwa ni kati ya wadaiwa sugu, Mchechu alisisitiza hakuna uhusiano wa siasa na zoezi hilo kwani wateja wote wanachukuliwa sawa.

“Mwaka huu ujenzi unaanza Dodoma," alisema Mchechu, hivyo fedha tunazodai zitatusaidia kukamilisha uwekezaji mjini humo."

“Ndiyo maana tumetoa kwa tunaowadai notisi ya miezi miwili, vinginevyo wataondolewa katika majengo ya shirika kama kanuni zinavyotaka.

“Hakuna uhusiano wowote kati ya shirika kukusanya fedha linazodai na watu binafsi akiwamo Mbowe, taasisi za umma na binafsi.

“Lengo ni kukusanya madeni ambayo baadhi yake yalisimama kutokana na mengine kuwa na kesi mahakamani.”

Alisema kuwa fedha hizo zitatumika kwa ujenzi wa nyumba za watumishi 300 hadi 500 mkoani Dodoma.

Alisema ujenzi huo unatarajia kuanza mara moja na utachukua miezi 12.

Kwa mujibu wa Mchechu, Sh. bilioni 60 za ujenzi wa nyumba hizo zitatokana na fedha za ndani.

Alisema shirika hilo limenunua ekari 240 eneo la Iyumbu, ekari saba Chamwino, nne Bahi na Chemba ekari nne pia ikiwa ni kuunga mkono azma ya Serikali ya Awamu ya Tano kuhamia Dodoma.

Alisema fedha nyingine zitapatikana baada ya nyumba 97 za shirika hilo zilizopo Medeli mjini Dodoma kuuzwa.

Aidha, Mchechu alisema kitendo cha Serikali kuhamia Dodoma kitatoa fursa kwa Jiji la Dar es Salaam kujiimarisha kibiashara tofauti na ilivyo sasa ambapo linakwamishwa na foleni kubwa za magari kutokana na shughuli nyingi za serikali kufanyika.

“Dar es Salaam kuna bandari, uwanja wa ndege," alisema na kuongeza: “Hivyo suala la kiuchumi litaimarika zaidi kutokana na shughuli nyingi za Serikali kuhamia Dodoma. Hii itasaidia uchumi wa nchi kusambaa katika maeneo tofauti nchini.”

Uwekezaji wa NHC jijini Dar es Salaam upo kwa asilimia 70, alisema na kwamba ufanisi wa Jiji utaongezeka hususani katika usafiri na sekta nyingine kiuchumi.

2 comments:

Anonymous said...

Wacha awe evicted.Hawa watu kwa muda mrefu walichukulia mali za serikali kama shamba la bibi.
Kama rent hailipiki vipi tax? sasa utaona ni kwanini kuna sanaa nyingi za kumzoretesha Magufuli ili asifanyekazi yake kikamilifu.

Anonymous said...

Sio hilo tu. Mbona hamzungumzii iliyokuwa EMBASSY HOTEL. Miaka na miaka imeendelea kuwa gofu tena katikati ya jiji. Hi ni aibu kubwa kwanini mmiliki wake halifanyii kazi na hata kama lina kesi mahakamani kwanini isimalizwe. Tusidanganyane..