Advertisements

Saturday, February 28, 2015

HABARI KAMILI YA MWALIMU WA KIKE ALIYEKUTWA NA KINYESI CHUMBANI KWAKE

Shehena ya kinyesi iliyokuwa chumbani kwa mwalimu huyo.
Pichani juu ni  Wafanyakazi wa usafi wa Manispaa ya Temeke wakibeba kinyesi kwenda kukimwaga baada ya kuvunja nyumba aliyokuwa akiishi Mwalimu Gaudencia Albert.
Mwandishi Wetu
HII ni simulizi ya aibu! Tukio la mwalimu wa Shule ya Sekondari ya Kibasila jijini Dar, Gaudensia Albert, mkazi wa Kisiwani Kata ya Sandali wilayani Temeke kuishi na vinyesi, mikojo na matapishi chumbani kwake, limeibua mshtuko na aibu ndani yake.

Kwa mujibu wa mwenye nyumba, Reuben Shayo, mwalimu huyo anayefundisha masomo ya sayansi aligundulika hivi karibuni kuwa anaishi ndani ya chumba chenye rundo la uchafu huo.
Shayo alifunguka: “Siku ya tukio (Februari 22, mwaka huu) tuliona funza wakitoka chini ya mlango wa ticha na harufu mbaya.

“Ukweli ni kwamba mwenzetu hatujawahi kumuona akioga wala akiingia chooni, ndiyo tukabaini uchafu huo baada ya kuchungulia ndani.
“Yaani hakuwahi kuleta mgeni wa aina yeyote na kumwingiza ndani hivyo inaonesha dhahiri alikuwa akiogopa kuonesha uchafu wake.”

Baada ya kugundulika kuwepo kwa uchafu huo, Shayo na wakazi hao walitoa taarifa polisi ambapo awali, Sajenti wa Jeshi la Polisi, Ramadhan Kagolo, aliwajibika kusimamia kuvunjwa kufuli la chumba hicho kwa vile kazi iliyokuwa ikifanyika ilikuwa ni kwa ajili ya kulinda afya ya jamii.
Jumatano iliyopita, Manispaa ya Temeke ilichukua uamuzi wa kuteketeza kinyesi kilichokutwa katika chumba cha mwalimu huyo baada ya maofisa wa afya wa manispaa hiyo kutaka kunusuru afya za wakazi wa eneo hilo.

Kazi hiyo ilifanyika majira ya saa 9:00 alasiri chini ya uangalizi wa jeshi la polisi kwa kushirikiana na mwenyekiti wa mtaa huo, Yahya Bwanga.
Wakati wa tukio hilo, Ofisa Afya wa Manispaa ya Temeke, Floyd Tembo alisema baada ya kupata taarifa za kuwepo kwa tukio hilo la kushangaza, waliwatuma watendaji wa afya wa kata hiyo wafanye utafiti wa kujua tatizo lina ukubwa gani.
“Baada ya kufanya utafiti wao pia walimpata mhusika ambapo tulichukua jukumu la kwenda kumhoji mkuu wa shule hiyo ili kujua kama mwalimu Gaudensia alikuwa na akili timamu au la.
“Hata hivyo, mkuu huyo wa shule alitueleza kuwa ana akili timamu na kwamba tukio hilo limewashtua walimu wenzake,” alisema Tembo.

Alisema pamoja na kuuteketeza mrundikano huo wa kinyesi, bado wanaendelea na utaratibu wa kumfikisha mwalimu huyo kwenye vyombo vya sheria ili kujua kwa nini alifanya hivyo.
“Hili tukio halihusiani na ugonjwa wa akili inawezekana kuna tatizo lingine au labda mambo ya ushirikina, haiwezekani ajisaidie na kuhifadhi uchafu ndani kwake,” alisema.
Alisema mwalimu huyo hakuweza kufika kwenye eneo la tukio hali iliyofanya mlango wa chumba chake uvunjwe chini ya uangalizi wa polisi.

Tembo alisema mwalimu huyo alishindwa kutokea kwenye eneo la tukio kwa vile alipelekwa Hospitali ya Temeke kisha kuhamishiwa Hospitali ya Taifa Muhimbili kwa ajili ya kupimwa afya baada ya kupata mshtuko ambao umesababishwa na taarifa hizo.
Afisa Afya wa Usafi wa Mazingira wa Temeke, Jumanne Muhogo alisema uchafu walioubaini ulikuwa ni uchafu wa kinyesi, mkojo na matapishi inasemekana kuna kipindi alikuwa anatapika.
“Tukio hili kwa Manispaa ya Temeke ni la kwanza kutokea, inaelekea huyu mtu hana akili ya kawaida kama angekuwa na akili ya kawaida asingeweza kufanya namna hii,” alisema.

GPL

No comments: